Tuesday, 30 April 2013


           NMB  YAKABIDHI MSAADA WA MADESKI   SKULI YA  BUMBWINI


Meneja Biashara  kutoka Makao Makuu ya Benki ya Biashara Jijini Dar es salaam Bibi Shilla Sennoro akimkabidhi Mgeni Rasmi Mama Asha Suleiman Iddi Madeski 100 na Viti 100 kwa ajili ya Skuli za Msingi za Bumbwini na Mangapwani hapo skuli ya Msingi Bumbwini Wilaya ya Kaskazini B.



Mama Asha Suleiman Iddi akikabidhi rasmi madeski 100 na Viti 100 kwa uongozi wa Skuli za Bumbwini na Mangapwani ambavyo vimetolewa msaada na Benki ya Biashara Tanzania { NMB } hapo Skuli ya Msingi Bumbwini Wilaya ya Kaskazini B.







Baadhi ya Wanafunzi wa Skuli ya Msingi ya Bumbwini na Mangapwani wakifurahia Vikalio vipya vilivyotolewa msaada na Benki ya Biashara Tanzania { NMB } hapo Skuli ya Msingi Bumbwini.

Picha  na Hassan Issa  (Vuga Newsroom )



 

 Press Release:-

Taasisi za Umma,Mashirika pamoja na Sekta Binafsi zina wajibu wa kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali Kuu katika kuwajengea mazingira bora Wananachi wake hasa katika Sekta muhimu ya Elimu yenye dhamana ya kufinyanga   wataalamu na Viongozi wa Baadae.
Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi alieleza hayo wakati wa hafla maalum ya kukabidhi Meza na Viti mia Moja kwa Skuli za Msingi za Bumbwini na Mangapwani iliyofanyika katika Skuli ya Msingi Bumbwini iliyopo Wilaya ya Kaskazini “ B”.
Msaada huo wenye thamani ya Shilingi za Kitanzania Milioni kumi                           { 10,000,000/- } umetolewa na Benki ya Biashara Tanzania { NMB } ambapo kila Skuli imebahatika kupata Meza Hamsini na Viti Hamsini.
Mama Asha Suleiman Iddi alisema  nguvu za Serikali pekee kwa sasa haziwezi kukidhi mahitaji ya Wananachi kutokana na kuongezeka kwa mahitaji miongoni mwa Wananchi na maeneo tofauti hapa Nchini.
Aliipongeza Benki ya Biashara Tanzania { NMB } kwa uamuzi wake wa kusaidia Sekta ya Elimu ambayo ndio muhimili mkubwa wa Maendeleo katika Taifa lolote Ulimwenguni.
Alisisitiza kwamba utekelezaji wa Sera ya Elimu Zanzibar katika kuhakikisha kila mtoto wa Taifa hili anapata Elimu ya lazima umo ndani ya Sera ya Chama cha Mapinduzi iliyopata ridhaa ya Wananchi walio wengi ilipokuwa  ikinadiwa wakati wa Kampeni za uchaguzi Mkuu uliopita wa Mwaka 2010.
Mke huyo wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  aliwaomba Wazaliwa na Vijiji hivyo  vya Bumbwini na Mangapwani kusaidia Maendeleo ya Vijiji vyao ili kuunganisha nguvu zao  pamoja na viongozi wao Mbunge na Mwakilishi.
Alishauri kufanywa kwa tathmini ili kujua  mahitaji halisi ya huduma za umeme ili kupata mbinu za  kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo  linalowakabili wananchi wa Mangapwani la ukosefu wa Huduma ya Umeme.
Mapema akitoa Taarifa fupi Meneja wa Biashara kutoka Makao Makuu ya Benki ya NMB Mjini Dar es salaam Bibi  Shilla Sennoro alisema anza ya Benki hiyo hivi sasa ni kuhakikisha inaimarisha huduma zake ili kwenda sambamba na jitihada za Serikali za kuwapatia huduma za kifedha wananchi walio wengi.
Bibi Shilla alieleza kuwa katika kutekeleza jitihada hizo Benki hiyo licha ya kuwa na matawi zaidi ya 145 Nchini kote lakini pia imelenga kuongeza mengine katika Wilaya mpya na maeneo mengine yanayohitaji huduma za kifedha.
Meneja huyo wa Biashara kutoka Makao Makuu ya NMB Jijini Dar es salaam alifahamisha kwamba hatua hiyo imelenga kusaidia wananchi kuokoa muda wao na kuutumia zaidi katika shughuli za kiuchumi.
Bibi Shilla Sennoro  alisema Taasisi yake kwa kutambua umuhimu wa Jamii na jitihada za Serikali Benki hiyo itaendelea kutoa misaada  kwa jamii katika sekta mbali mbali kadri hali itakavyoruhusu.
Katika Risala yao Wananchi, Walimu na Wanafunzi hao wa Vijiji vya Bumbwini na Mangapwani wameishukuru Benki ya Biashara ya NMB kwa uwamuzi wake wa kusaidia Samani skuli hizo ambazo zipapunguza kero linalowakabili wanafunzi la baadhi yao kukaa chini.
Hata hivyo wananchi, walimu na Wanafunzi hao walisema  bado skuli hizo zinaendelea kukabiliwa na changa moto kadhaa ikiwemo huduma za maji safi, Umeme kwa kijiji cha mangapwani pamoja na uchakavu wa baadhi ya Majengo ya Skuli zao.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
30/4/2013.



Saturday, 27 April 2013




 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa pamoja na Ujumbe wa Viongozi wa Makampuni ya Maji na Umeme               { Botjheng Water na Megtron } ya Afrika Kusini pamoja Uongozi wa Wizara ya Ardhi , Makazi, Maji na Nishati aliokutana nao Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.







Mwakilishi wa Makampuni ya Botjheng Water na Megatron ya Afrika Kusini Bwana Dean Hiran  akiwa  pamoja na Viongozi wa Makampuni hayo wakizungumza na Uongozi wa Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati chini ya Uenyekiti wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa katika Picha ya pamoja na Uongozi wa Makampuni ya Maji na Umeme { Botjheng Water na Megatron } ya Afrika Kusini mara baada ya kumaliza mazungumzo yao.
Picha nan Hassan Issa wa – OMPR – ZNZ.




Wednesday, 24 April 2013


Mbunge wa Jimbo la Kitope Balozi Seif Ali Iddi akiwa na Mkewe Mama Asha Suleiman Iddi wakisikiliza Taarifa fupi iliyosomwa na Katibu wa Kamati ya Maendeleo ya Kijiji cha Vuga Mkadini Nd. Hamad Mwinyi Ramadhan katika uzinduzi wa Mradi wa maji safi na salama wa Kijiji cha Vuga Mkadini.



Mbunge wa Jimbo la Kitope Balozi Seif Ali Iddi akizindua mradi wa maji safi na salama katika Kijiji cha Vuga Mkadini ndani ya Jimbo la Kitope.
Nyuma ya Balozi Seif ni Mkewe Mama Asha Suleiman Iddi pamoja na baadhi ya wananchi walioshuhudia uzinduzi huo.

Picha na Hassan Issa wa  - OMPR – ZNZ.

 Press Release:-
Uongozi wa Jimbo la Kitope umekusudia kujitahidi katika kuhakikisha huduma za Maji safi na salama ndani ya Jimbo hilo zinapatikana ili kuwaondoshea usumbufu wa huduma hiyo Wananchi wake.
Mbunge wa Jimbo hilo Balozi Seif alieleza hayo wakati akizindua mradi wa huduma za maji safi na salama katika kijiji cha Vuga Mkadini kilichomo ndani ya jimbo la Kitope.

Balozi Seif ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema Maji ni miongoni mwa huduma muhimu inayopaswa kutumiwa na kila mwanaadamu, hivyo Uongozi huo utachukuwa juhudi ya ziada katika kuona kero za upatikanaji wa huduma hiyo inakuwa ndoto ndani ya jimbo hilo.
Aliwaeleza Wananchi hao wa Kijiji cha Vuga Mkadini kwamba utaratibu mwengine utaangaliwa katika mpango wa kujenga Tangi jengine katika eneo hilo ili lisaidie kukidhi mahitaji ya maji ambayo kwa hivi sasa yanaendelea kuwa ya mgao.
Balozi Seif aliwakumbusha Wananchi hao kuzingatia maagizo ya Wahandisi katika matumizi ya mashine zinazotumika katika Tangi la Kisima kilichopo Kijijini hapo ili zidumu kutoa huduma kwa muda mrefu zaidi.

Akitoa Taarifa ya uzinduzi wa Mradi wa maji safi na salama wa katika Kijiji hicho cha Vuga Mkadini Katibu wa Kamati ya  maendeleo ya Kijiji hicho Ndugu  Hamad Mwinyi Ramadhan alisema huduma za maji safi ilikuwa ni kilio cha muda mrefu katika kijiji chao.
Nd. Hamadi alisema juhudi za Viongozi wa Jimbo hilo kupitia Mbunge huyo katika harakati za ziada za kujituma zimesaidia kuleta maendeleo ya haraka ndani ya Jimbo  hilo.
“ Ukweli juhudi unazoendelea nazo siku hadi siku, hasa kilio chetu cha ukosefu wa Pump ya kupandisha maji na Switch Control Box zimeleta faraja na kwa kweli tunajisikia raha isiyo kifani “. Alisema Katibu wa Kamati ya Maendeleo ya Kijiji cha Vuga Mkadini Nd. Hamad.
Akitoa Shukrani kwa niaba ya Wananachi wa Kijiji hicho Diwani wa Wadi ya Fujoni Nd. Hamad Khamis Hamad amempongeza Mbunge wa Jimbo hilo Balozi Seif kupitia uratibu wa Mke wake Mama Asha Suleiman Iddi kwa kusimamia vyema maendeleo ya Wananachi wa Jimbo hilo.

Diwani Hamad alisema Wananchi wa Jimbo hilo wamekuwa wakishuhudia usimamizi wa Mbunge Kimawazo na hata uwezeshaji unaoendelea kuleta faraja na neema kwa wananchi hao.
Mbunge wa Jimbo la Kitope Balozi Seif tayari ameshauzindua mradi wa Maji safi na Salama wa Kijiji cha Kipandoni uliogharimu shilingi Milioni 2,300,000/-, Kisima cha Maji Mgambo kiligharimu shilingi Milioni 4,000,000/- na mradi wa Vuga Mkadini umegharimu zaidi ya Shilingi Milioni 6,900,000/-.
Miradi yote mitatu imegharimu zaidi ya shilingi Milioni Kumi na Tatu na Laki Mbili { 13,200,000/- }.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
24/4/2013.




Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na watendaji wa shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC } alipofanya ziara ya ghafla Kituoni hapo Karume House


 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiwa pamoja na Uongozi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo pamoja na ule wa ZBC wakisikiliza changamoto za watendaji wa ZBC wakati alipofanya ziara fupi kituoni hapo


 Baadhi ya watendaji wa Shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC } wakisikiliza hotuba ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi hayupo pichani alipofanya ziara fupi Kituoni hapo.


 Mhandisi wa ZBC Saadat Haji akielezea kero wanazopambana nazo Kituoni hapo mbele ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliyefanya ziara ya ghafla Kituoni hapo.



 Mtayarishaji wa Vipindi shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC } Nasra Nassor akishauri umuhimu wa kuwa na bajeti maalum katika utengenezaji wa vipindi.




Press Release:-
Matumaini ya Wananachi katika kupokea na hatimae kuangalia matangazo ya Televisheni kupitia Shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC } yatarejea endapo watendaji wa Shirika hilo kwa kushirikiana na Viongozi wao watajipanga vyema katika kutekeleza majukumu yao.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo alipofanya ziara ya ghafla katika Kituo cha Televisheni cha Shirika hilo kilichopo Karume House kuangalia matatizo yaliyopelekea kukosekana kwa matangazo ya Habari Kituoni hapo.

Akizungumza na Uongozi wa Shirika hilo na baadae Watendaji wake Balozi Seif alisema Serikali iliamua kuunda Shirika hilo lengo likiwa ni kuimarisha zaidi matangazo yake pamoja na kwenda sambamba na mabadiliko ya mfumo wa utendaji katika sekta ya Habari Duniani.
Balozi Seif alisisitiza kwamba wakati umefika hivi sasa   kwa Shirika hilo kuendeshwa kibiashara, na hilo litafikiwa iwapo Taasisi zinazoendelea na zile zinazotumia na kuhitaji huduma za matangazo za Shirika hilo zitalipa.
“ Sisi Serikalini tumeshaliagiza Baraza la Wawakilishi ambalo liko chini ya Wizara yangu lianze kulipa fedha wakati linapoendelea na vikao vya Baraza katika matangazo yake ya moja kwa moja. Dodoma Shirika la Utangazaji Tanzania TBC wanalipwa na Bunge wakati wanaporusha matangazo yao utaratibu ambao hata sisi wabunge tunachangia suala hilo “. Alifafanua Balozi Seif.
“ Katika kujenga mahusiano mema baina ya Taasisi hizo inaweza kuruhusiwa kutangazwa  bure wakati wa kipindi cha maswali na majibu “. Alisisitiza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Akizungumzia suala la uwajibikaji Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliwaonya watendaji hao kuwepuka tabia ya fitna baina yao na Viongozi jambo ambalo linarejesha nyuma ufanisi wa kazi zao.
Alikemea kwamba Kiongozi ye yote ambae atapenda kutanguliza fitna na majungu mbele aelewe kwamba anajiingiza katika mfumo mbaya wa kazi unaosababisha kuyeyusha haki za wafanyakazi wake.

Hata hivyo Balozi Seif aliwapongeza Watendaji wa Shirika la Utangazaji Zanzibar { ZBC } kwa utendaji wao wa kizalengo licha ya kukabiliwa na mazingira magumu ya utekelezaji wa majukumu yao waliyopangiwa.
Mapema Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Utangazaji Zanzibar Nd. Chande Omar Omar alisema Vituo vya Matangazo ya Televisheni haviwezi kufanya kazi zake kwa mpangilio wa bajeti kama zinavyofanya Idara nyengine.
Alisema Uongozi wa Shirika hilo umekuwa akitoa Taarifa za maandishi wakati yanapotokea matatizo hasa suala kubwa la vifaa na uharibikaji wa mashine lakini ufumbuzi wake huchukuwa muda mrefu kutokana na mfumo wa matumizi uliopo.
“ Tumekuwa tukiiandikia Wizara kuijuilisha matatizo yetu yanapotokea lakini hatua zinazochukuliwa za kusubiri fedha hupelekea hata vile vifaa vya dharura vikaharibika baada ya kukosa usaidizi wa ziada “. Alisema Kaimu Mkurugenzi huyo wa ZBC Nd. Chande.

Hata hivyo Ndugu Chande alimueleza Balozi Seif kwamba Uongozi wa Shirika hilo tayari umeshachukuwa hatua za dharura kukabiliana na tatizo hilo kwa kuwasiliana na makampuni yanayotengeneza vifaa vinavyohitajika kituoni hapo kwa wakati huu wa dharura.
Alisema lengo la Shirika hilo katika mpango wake wa kuingia katika matangazo ya Kisasa ya Digital ni kuwa na mashine 10 za kurikodia vipindi zitakazotosheleza kabisa mahitaji ya vitengo vya Habari, Vipindi pamoja na Matangazo.
Kwa upande wao watendaji wa shirika hilo la Utangazaji Zanzibar wameelezea changamoto wanazopambana nazo kituoni hapo ambazo zimekuwa zikirejesha nyuma hamu na utendaji wao wa kazi za kila siku.

Walizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na ukosefu usafiri wa uhakika wa kufuatilia Vipindi, Habari na hata kurejeshwa majumbani wakati wa usiku, ukosefu wa Bajeti za Vipindi, uchakavu wa Mashine za Matangazo, Haki za Wafanyakazi kama maposho na fedha za likizo pamoja na majungu na fitina baina ya Viongozi na Wafanyakazi.


Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
24/4/2013.






Press release

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imemuagiza mwekezaji aliyepewa eneo la Magofu ya Kihistoria liliopo Bweleo Wilaya ya Magharibi kuhakikisha kwamba ameshakamilisha shughuli zake za uwekezaji na kuanza kutoka huduma kama alivyoahidi katika mkataba wake ndani ya kipindi cha Mwaka mmoja kuanzia leo.
Agizo hilo limetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akizungumza na Mwekezaji huyo Bwana Chandra, Katibu wa Kamati ya Maendeleo ya watu wa Bweleo, Sheha wa Shehia ya Bweleo, Mkurugenzi Zipa pamoja na  Mkurugenzi Mazingira hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.

Balozi Seif alisema ameridhika na mapendekezo yaliyotolewa na Kamati Maalum aliyoiteua kuchunguza mgogoro wa eneo hilo Tarahere 28 Oktoba mwaka 20112 kati ya Mwekezaji huyo na wananachi wa Bweleo waliyoiomba Serikali Kuu kumnyang’anya eneo hilo Mwekezaji huyo baada ya kukaa nalo kwa miaka mingi bila ya faida ya Wananchi hao.
Akifafanua baadhi ya mapendekezo yaliyotolewa na Kamati hiyo Maalum ya kuchunguza mgogoro wa eneo hilo  ambayo iliongozwa na Mkuu wa Mkoa Mjini Mgharibi Mh. Abdulla Mwinyi, Balozi Seif alimtaka Mwekezaji huyo kuhakikisha kwamba mradi wake unafaidisha kimapato Wananchi wa maeneo hayo.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema njia pekee ya kuepuka migogoro ndani ya sekta ya uwekezaji ni kwa wananchi wenyewe kuiachia Serikali kuu kutimiza waji wake kwa kutiliana saini ya mikataba na wawekezaji ili kuwepuka ujanja unaopelekea kuleta mzozo hapo baadaye.
“ Moja kati ya suala nililolishuhudia wakati wa ziara yangu mwaja jana katika eneo hilo ni lile lalamiko la wananchi hao la kuzibiwa njia wanayoitumia wakati wanapotoka katika shughuli zao za uvuvi. Hili unapaswa kulichukulia hatua mara moja kwa kushirikiana na Uongozi wa Shehia, Zipa na Mazingira “. Balozi Seif alimuagiza Mwekezaji huyo.
Hata Hivyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimpongeza Mwekezaji huyo Bwana Chandra kwa hatua yake ya kusaidia maendeleo ya Wananachi wa Vijiji vinavyouzunguuka mradi huo na kumuomba asichoke kuendelea kufanya hivyo ili kujenga uhusiano mwema na Wananchi hao.

Balozi Seif aliusisitiza Uongozi wa mradi huo kuwasiliana na Taasisi ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar { ZIPA }, Mipango Miji pamoja na Idara ya Mazingira ili kuhakikisha kwamba mradi huo unaendeshwa katika misingi iliyokubalika kutekelezwa Kisheria.
Eneo la Magufu ya Kihistoria la Bweleo limekuwa na mzozo wa muda mrefu kati ya Mwekezaji wake Bwana Chandra na Wananchi wa Vijiji vilivyolizunguuka eneo hilo wakidai Mwekezaji huyo kushindwa kuliendeleza kama ilivyokubalika.


Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu Pili wa Rais wa Zanzibar
23/4/2013..

Monday, 22 April 2013


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akizindua wiki ya usalama bara barani hapo katika ukumbi wa salama hoteli ya bwawani Mjini Zanzibar.

Amina Mkombe na Mwanajuma Mkombe wakisoma utenzi kusherehesha kwenye usinduzi wa wiki ya usalama bara barani zilizofanyika katika ukumbi wa salama katika hoteli ya Bwawani Mjini Zanzibar.


Kamishna wa Polisi Zanzibar Mussa Ali Mussa akitoa takwimu za ajali na vifo kwa mwaka 2012 na 2012 kwenye uzinduzi wa wiki ya usalama bara barani zilizofanyika katika ukumbi wa salama  bwawani hoteli.





Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dr. Saleh Mohammed Jidawi akitoa takwimu za vifo na majeruhi waliopokelewa katika vituo mbali mbali vya afya hapa Zanzibar kwenye uzinduzi wa wiki ya usalama bara barani hapo bwawani hoteli.




Mwakilishi wa Wizara ya elimi Zanzibar Bwana  Ahmed Abdull majid akielezea madhara wanayoyapata wanafunzi waendapo maskulini wakati wanapotumia bara bara kwenye uzinduzi wa wiki ya usalama bara barani hapo bwawani Hoteli.




Katibu Mkuu Wizara ya Miundo Mbinu na Mawasiliano Dr. Juma  Malik akielezea juhudi zinazochukuliwa na Wizara yake katika kuendeleza miundo mbinu ya bara bara ili kupunguza ajali.




Waziri wa MKiundo Mbinu na Mawasiliano Zanzibar Mh. Rashid Seif akizungumza katika uzinduzi wa wiki ya usalama bara barani hapo Hoteli ya Bwawani Mjini Zanzibar.




Baadhi ya washiriki walioshuhudia uzinduzi wa wiki ya usalama bara barani zilizofanyika katika ukumbi wa salama hoteli ya bwawani Mjini Zanzibar.



Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Kudumu ya usalama bara barani Mh. Abdulla Mwinyi ambae pia ni Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi akitoa shukrani mara baada ya kumalizika kwa uzinduzi wa wiki ya usalama wa bara barani hapo bwawani Hoteli Mjini Zanzibar.

 Picha Hassan Issa wa  - OMPR – ZNZ.


  Press Release:-

Wananchi wanaotumia  usafiri wa dala dala na magari yaendayo vijijini wametakiwa kuchukua hatua za kuripoti katika vituo vya Polisi au Idara ya Usafiri na leseni mara moja dhidi ya Madereva au Matingo  wanaowafanyia  vitendo vinavyokiuka sheria za bara barani.
Hatua ya kukomesha vitendo hivyo kwa kuchukuliwa hatua kali za kisheria  wahusika hao zitafanikiwa vyema endapo Wananchi watakubali kutoa ushirikiano unaofaa kwa Taasisi hizo katika kukabiliana na usumbufu huo.
Wito huo umetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akizindua rasmi Wiki ya Usalama Bara barani hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Salama uliopo Hoteli ya Bwawani Mjini Zanzibar.

Balozi Seif aliliamuru Jeshi la Polisi, Kikosi cha usalama bara barani kusimamia sheria za usalama bara barani na kuondoa muhali kwa wote wanaokiuka sheria hizo kwa kuwachukuliwa hatua kali za kisheria kwani hakuna mtu aliyekuwa juu ya sheria.
Alisema kwa kuwa suala la usalama wa bara barani linahitaji nguvu za pamoja  madereva wana wajibu wa kuwajali watumiaji wengine wa bara bara ikiwa ni pamoja na watembeao kwa miguu, wapanda baskeli wakiwemo pia watu wenye mahitaji maalum.

Balozi Seif alielezea masikitiko yake kutokana na baadhi ya madereva na Matingo wao  kuwanyanyasa wananchi ambao ndio abiria wao kwa kutowafikisha  mwisho wa safari kama walivyoomba ruhusa ya usafirishaji pamoja na kuwatolea lugha chafu.
Akizungumzia suala la matumizi mabaya ya bara bara Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alisema bara bara nyingi zinaharibiwa  kwa kuwekwa matuta na wananchi baaba ya kukosa imani ya uendeshaji mbovu unaofanywa na baadhi ya madereva.
Balozi Seif alionya kwamba wakati umefika kwa Taasisi inayosimamia masuala ya Leseni kuweka utaratibu wa  kuwanyang’anya Leseni Madereva wanaosababisha  ajali  za mara kwa mara kwa makusudi na  uzembe.

Aliitaja sababu moja kubwa inayochangia ajali za mara kwa mara kwenye bara bara  nyingi hapa nchini kuwa ni matumizi ya simu za mkononi hali inayomfanya Dereva kufanya mambo mawili kwa wakati mmoja.
“ Haiwezekani kuchanganya mambo mawili kwa wakati mmoja. Na hili tumekuwa tukilishuhudia pia ndani ya majengo ya ibada ambapo muumini anashindwa kuzima simu yake wakati tayari mlangoni pameshawekwa tangazo la kukumbusha jambo hilo “. Alifafanua Balozi Seif.

“ Ukweli usiofichika ni kwamba Jamii kubwa ya Wazanzibari imekuwa kaidi katika kutii sheria ambazo zimetungwa maalum kwa lengo la kufuatwa uadilifu utakaotoa haki kwa kila Mtu “. Alisisitiza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Akigusia tukio la uzinduzi wa wiki ya usalama bara barani ikiwa ni sehemu ya kutathmini utekelezaji wa mpango wa miaka kumi ya usalama bara barani ulioanzishwa na Rais wa Zanzibar Dr. Sheni Disemba mwaka 2011 Balozi Seif alisema  ajali za bara barani zimefikia kushika nafasi ya Pili kwa kusababisha vifo vingi baada ya ugonjwa wa ukimwi.
Hata hivyo Balozi Seif alifahamisha kwamba uelewa wa hali ya usalama bara barani duniani umeongezeka baada ya shirika la Afya Ulimwenguni { WHO } kueleza kuwa watu wapatao Milioni 1.3 hufa na wengine wapatao Milioni 50 hujeruhiwa ulimwenguni kila mwaka.
Alieleza kwamba ajali ya bara barani zina athari kiuchumi kwa kupunguza nguvu kazi ya Taifa sambamba na kuwaacha watu wenye ulemavu ambao kwa kiasi kikubwa  hupunguza uwezo wao wa uzalishaji mali katika kujipatia kipato kinachowawezesha katika maisha yao ya kila siku.

Balozi Seif alisema katika kukabiliana na changa moto hiyo ya ajali za bara barani Serikali itahakikisha inasimamia vilivyo bara bara zinazojengwa  ili zikidhi viwango ikiwa ni pamoja na uimara wa bara bara zenyewe, upana, pamoja na kuwekwa kwa alama za bara barani.
Mapema Kamishna wa Polisi Zanzibar Bwana Mussa Ali Mussa alisema Jeshi la Polisi linaendelea kuchukuwa hatua mbali mbali ili kupunguza ajali zinazosababishwa na ubovu wa magari pamoja na madereva wazembe.

Kamishna Mussa alisema ajali za bara barani kwa mwaka 2012 zilifikia 855 ikilinganishwa na ajali 849 kwa mwaka 2011 ikiwa na ongezeko la ajali sita wakati ambapo ajali hizo zimesababisha vifo vya watu 138 kwa mwaka 2012 kukiwa na ongezeko la vifo vya watu 47 ikilinganishwa na vile vya mwaka 2011 vya watu 117.
Bwana Mussa alizishauri Taasisi zinazohusika kuweka viwango maalum vya uingizaji wa magari nchini  kupunguza vyombo vilivyochakaa ambavyo ndivyo vinavyochangia kuongezeka kwa msongamano wa ajali zinazotokea Nchini.
Kamishna Mussa alisisitiza umuhimu wa kutumiwa kwa utatu ambao ni mawasiliano, mashirikiano pamoja na Uratibu katika kufanikisha malengo ya matumizi bora ya sheria ikiwemo  suala la matumizi sahihi ya bara bara.

Wakitoa mawazo yao baadhi ya wajumbe wa Kamati hiyo ya wiki ya usalama bara barani walisema ajali zinaweza kupungua au kuondoka kabisa iwapo alama za bara barani zitatumiwa kama zilivyokusudiwa.
Walisema wakati busara inaweza  kuokoa ajali kwa suala hili kuwekwa katika vichwa vya madereva wakati umefika kwa Wizara ya Maiundo mbinu na mawasiliano kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kulijadili tatizo la matumizi ya simu unaofanywa na madereva wakati wanapoendesha gari bara barani.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
22/4/2013.





 HOTUBA YA MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR,
 MHE. BALOZI SEIF ALI IDDI YA KUAHIRISHA MKUTANO WA KUMI NA MOJA WA BARAZA LA
                                           WAWAKILISHI- TAREHE 19 APRILI, 2013

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwenye wingi wa rehema na neema, kwa kutujaalia uzima na afya njema tukaweza kuhudhuria Mkutano huu wa kumi na moja wa Baraza lako Tukufu. Nakushukuru wewe Mheshimiwa Spika na wasaidizi wako wote.  Kama kawaida yako umeliendesha vyema Baraza hili na kwa umahiri mkubwa, hekima na busara ambazo zimefanikisha mkutano huu.   Mafanikio ya mkutano huu pia yanatokana na umakini wa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kwa michango yao mbali mbali waliyoitoa wakati wote wa majadiliano.

Mheshimiwa Spika, mchango wa waandishi wa habari pia ni mkubwa katika kufanikisha mkutano huu.  Kwa kipindi chote cha mkutano wetu vyombo vya habari vya Serikali na watu binafsi vimekuwa vikifuatilia kwa karibu majadiliano yetu na hatimaye kuwafikishia wananchi wetu.  Hongereni sana kwa kazi yenu nzuri.
Mheshimiwa Spika, namshukuru kwa dhati Rais wetu mpendwa wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, kwa busara, hekima na ujasiri mkubwa alionao katika kuliongoza Taifa letu na kutuletea maendeleo. Ni dhahiri kwamba, wananchi wa Zanzibar wamekuwa na imani na matumaini makubwa kwa Rais wao kutokana na mabadiliko yanayoonekana katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii. Aidha, namshukuru na kumpongeza Makamu wa Kwanza wa Rais, Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad kwa jitihada kubwa anayochukua kumshauri vizuri Rais wetu katika kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Sina budi pia kuwashukuru Viongozi wote wa Serikali, Vyama vya Siasa na wananchi kwa ujumla kwa namna wanavyoendelea kudumisha amani na utulivu na kutekeleza majukumu yao katika kuleta maendeleo ya nchi yetu. Ni matumaini yangu kwamba watauendeleza mwenendo huu ili amani na utulivu viendelee kutawala katika nchi yetu, kwani bila ya amani na utulivu maendeleo tunayotafuta yatakuwa taabu kupatikana.

MASUALA MUHIMU YALIYOJIRI NCHINI:
Mheshimiwa Spika, tarehe 24 Machi, 2013 nchi yetu ya Tanzania ilipokea ugeni wa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Xi Jinping ambapo lengo kubwa la ziara hiyo ni kukuza uwekezaji wa biashara baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China. Aidha, Rais wa China alipata nafasi ya kuzungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pamoja na Viongozi Waandamizi wa SMZ. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imenufaika kwa kiwango kikubwa na ziara ya Rais Xi Jinping ambapo jumla ya miradi saba (7) imo kwenye mpango wa kunufaika na ufadhili wa Serikali ya China. Kati ya miradi hiyo saba (7), miradi mitatu (3) imekubaliwa kupewa fedha ikiwemo mradi wa kazi za miundombinu, ukarabati wa matengenezo ya Hospitali ya Abdalla Mzee na kupatiwa msaada wa vifaa vya kukagua mizigo iliyomo ndani ya kontena bandarini.  Namshukuru sana Mheshimiwa Omar Yussuf Mzee, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo kwa kuliarifu Baraza lako Tukufu kwa ukamilifu kuhusu ugeni huu.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyoelewa kuwa hivi sasa tuko katika kipindi cha msimu wa mvua za masika. Mwishoni mwa mwezi wa Februari 2013, Mamlaka ya Hali ya Hewa ya Tanzania Kanda ya Zanzibar ilitoa taarifa ya mwelekeo wa mvua za masika kwa mwaka huu ambayo ilielezea kuwa mvua hizo zilitarajiwa kuanza mapema kuliko kawaida na zingekuwa za wastani na juu ya wastani kwa mwezi wa Machi na kutarajiwa kuwa chini ya wastani kwa miezi ya Aprili na Mei. Baada ya kupokea taarifa hiyo, Kamati ya Taifa ya Kukabiliana na Maafa ilijadili na kuweka mikakati na hatua madhubuti za kuchukuliwa ili mvua hizo pindipo zikinyesha, zisiweze kuleta madhara makubwa. Kamati iliziagiza sekta zote zinazohusika na kukabiliana na maafa ziendelee kuchukua hatua za tahadhari na kujiandaa kukabiliana na majanga pindipo yakitokezea.  Mpaka sasa tunamshukuru Mwenyezi Mungu kuwa hali ya wananchi wetu bado iko salama na hakuna madhara makubwa yaliyokwisha tokea.  Aidha, mvua za mwaka huu zimekuwa zikinyesha vizuri, kwani zimekuwa zikitupa muda wa kujitafutia riziki.
Mheshimiwa Spika, nchi yetu imo katika harakati za kupata Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tume iliyoundwa ya Kukusanya na Kuratibu Maoni ya Mabadiliko ya Katiba kutoka kwa wananchi tayari imekamilisha kukusanya maoni hayo kupitia Shehia zao, Taasisi za Serikali na zisizokuwa za Serikali pamoja na makundi maalum. Hii ilikuwa ni hatua ya kwanza. Hivi sasa kazi ya uundaji wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya, ikiwa ni hatua ya pili inaendelea ambapo Mabaraza hayo yataanza kazi zake za kupitia Rasimu ya awali ya Katiba Mpya hivi karibuni. Ni imani yangu kwamba, Mabaraza hayo yatatekeleza majukumu yao kwa umakini na ufanisi kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa. Nitumie nafasi hii kuwasihi Wajumbe wa Mabaraza hayo kuitumia fursa hiyo muhimu na ya kipekee kutoa michango yenye maslahi ya nchi yetu na wananchi wake bila kuweka mbele itikadi zao za Vyama vya Siasa, dini na maeneo wanayotoka.  Naamini kuwa kama ilivyomalizika hatua ya kwanza, na hatua hii ya pili itamalizika salama.

Mheshimiwa Spika, siku ya tarehe 10 Aprili, 2013 Wazanzibari sote tulijumuika katika sherehe za Uzinduzi wa kukamilika mradi wa njia mpya ya kusafirishia umeme yenye uwezo wa kuchukua Megawati 100 za umeme kutoka Dar es Salaam hadi Zanzibar ambapo Mgeni Rasmi alikuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Ali Mohamed Shein. Kwa hakika nchi yetu imefungua ukurasa mwengine wa maendeleo katika nyanja hii muhimu kwa mustakbali wa maendeleo yetu ya kiuchumi na kijamii. Hatua hii ni muendelezo wa azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuimarisha upatikanaji wa huduma ya nishati ya umeme hapa Zanzibar kama ilivyoelezwa katika Dira yetu ya Maendeleo ya 2020, Mpango wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA II) na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010 – 2015. Tunatoa pongezi na shukurani za dhati kwa Serikali na Watu wa Marekani kupitia Mfuko wa Changamoto za Milenia (MCC) kwa kutuunga mkono katika jitihada zetu za kujiletea maendeleo hasa katika mradi huu na ule wa ujenzi wa barabara za Kaskazini, Pemba. Napenda kutoa wito kwa wananchi kuthamini jitihada hizi za Serikali kwa kuilinda na kuitunza miundombinu yote ya umeme huu na ile ya awali kwa kuhifadhi mazingira ya maeneo ambayo miundombinu hiyo imepita.  Kwa kuupata umeme huu, tunatumai kauli ya Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati kuwa mgao wa umeme sasa basi itakuwa ya kweli.  Pamoja na kuupata mradi huu muhimu, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea na juhudi zake za kuwakaribisha wawekezaji wenye nia ya kuja kuwekeza katika miradi ya nishati mbadala ili kuongeza uwezo wa Zanzibar kuwa na umeme wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, taarifa za kitaalamu juu ya ugonjwa wa malaria hapa nchini inaonesha kwamba kwa kiasi kikubwa ugonjwa huu umedhibitiwa kupitia Programu ya Kupambana na Malaria inayofadhiliwa kwa pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Marekani. Hata hivyo, bado kuna matukio machache ya kupatikana wagonjwa katika Wilaya tisa (9) za Unguja na Pemba. Ni Wilaya ya Mjini pekee ambayo hadi sasa haijaripotiwa kupatikana mgonjwa wa malaria. Serikali imeendelea na kazi ya upigaji dawa katika maeneo yaliyobainika kuwepo wagonjwa wa malaria. Jumla ya nyumba 26,900 zimepigwa dawa kati ya nyumba 28,463 sawa na asilimia 94.5 ya nyumba zote zilizotakiwa kupigwa dawa.  Aidha, jumla ya wagonjwa wanne (4) wa malaria Unguja na Pemba wameripotiwa kufariki katika kipindi cha Julai, 2012 hadi Machi, 2013. Natoa wito kwa wananchi kuendelea kutumia vyandarua vilivyowekwa dawa pamoja na kutoa mashirikiano kwa watendaji wanaosimamia zoezi la upigaji dawa majumbani ili kushinda vita dhidi ya malaria, kwani Zanzibar bila malaria inawezekana. Pamoja na juhudi hizo za Serikali, bado kuna baadhi ya wananchi wakiwemo na baadhi ya Viongozi kukataa nyumba zao kupigwa dawa. Ningewasihi sana wananchi na hasa viongozi kuacha tabia hiyo ili wawe mfano kwa wananchi wengine.

Mheshimiwa Spika, katika siku za hivi karibuni nchi yetu imeshuhudia matukio mbali mbali ya majanga hasa kuungua kwa majengo ya makaazi na biashara, matukio ambayo yanarudisha nyuma ustawi na maendeleo ya wananchi na Taifa kwa jumla. Uzoefu unaonesha kwamba, wananchi wanaofikwa na matatizo hayo mara nyingi hushindwa kurudi katika hali zao za kawaida kwa haraka na hivyo hupelekea kukata tamaa na shughuli zao za kiuchumi na kupata makaazi bora. Ni vyema basi wananchi na wafanya biashara wetu kuwa na utamaduni wa kukata bima ili kulinda mali zao majumbani na sehemu za biashara. Aidha, nawaomba Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako kutumia nafasi zao kushajiisha jamii katika maeneo yao juu ya umuhimu wa kukata bima. Ni jambo la kustaajabisha kuona mwananchi anaikatia bima gari yake yenye thamani ya Shilingi Milioni 5 au 10, lakini anaacha kukatia bima nyumba yake au sehemu yake ya biashara yenye thamani kubwa zaidi ya hapo. Nawaomba wananchi waitumie fursa zinazotolewa na Mashirika ya Bima ili kulinda mali zao.
Mheshimiwa Spika, ardhi ni rasilimali muhimu katika maendeleo ya nchi na wananchi wake kiuchumi na kijamii. Kwa mujibu wa sheria, rasilimali hii bado itaendelea kuwa mali ya Serikali. Hivyo, wananchi na Taasisi zitapewa ardhi kwa matumizi yao tu na haitoruhusiwa kuuzwa. Hata hivyo, kumejitokeza tabia ya wananchi na baadhi ya Viongozi kuuza ardhi kiholela bila kufuata sheria na taratibu ziliopo hali ambayo inasababisha migogoro. Serikali haitomvumilia mtu yeyote atakaekwenda kinyume na sheria na taratibu hizo. Kama kila mara Mheshimiwa Rais anavyotukumbusha kuwa ardhi ni mali ya Serikali na haipaswi kuuzwa. Mtu anaeuza ardhi anauza mali ambayo siyo yake.  Hivyo, muuzaji na mnunuzi wote kwa pamoja ni wakosaji na wanapaswa kuadhibiwa kwa mujibu wa taratibu zilizopo. Naielekeza Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati kuisimamia vyema sheria za ardhi bila ya kumuonea haya mtu yeyote.  Naipongeza Kamati ya Mawasiliano na Uchukuzi kwa kutukumbusha kuwa ardhi ambayo imetengwa kwa ajili ya maendeleo ya jamii iachwe itumike kwa shughuli hiyo.  Lakini pia na wale wananchi waliopewa maeneo makubwa yapunguzwe ili wananchi wengine nao wafaidike na rasilimali yao hii.  Namuagiza Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati ayatekeleze maelekezo hayo.
Mheshimiwa Spika, katika kulitafutia ufumbuzi wa kudumu suala la migogoro ya ardhi, Serikali imeona njia pekee na nzuri ni kusajili ardhi kwa utaratibu uliowekwa na Sheria Namba 10 ya mwaka 1990. Katika utaratibu huo, kutakuwa na mfumo maalum wa kuwatambua watumiaji wa ardhi kama vile; waliopewa eka tatu tatu, mashamba binafsi, mashamba ya Serikali na maeneo ya wazi. Hivyo, nachukua nafasi hii kuwataka wananchi wote kusajili ardhi wanazozitumia katika muda uliopangwa kupitia Ofisi ya Mrajisi wa Ardhi ili kuepusha usumbufu unaoweza kujitokeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanzisha Sheria ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo ya mwaka 2012 kwa lengo la kuhakikisha kuwa inapeleka maendeleo na huduma mbali mbali za jamii karibu na wananchi wa visiwa vyetu vya Unguja na Pemba. Fedha hizo tayari zimeshakabidhiwa kwa Waheshimiwa Wajumbe wote wanaostahiki kwa mwaka 2012 ambazo zilikuwa ni Shilingi Milioni Kumi (Shs:10,000,000/=) kwa kila mmoja. Ni mategemeo ya Serikali kwamba fedha hizo zimetumika kwa mujibu wa matakwa ya sheria husika. Kwa mwaka huu 2013 Serikali imeamua kuongeza kima hicho cha Shilingi Milion 10 hadi kufikia Milioni 15 ili kuwawezesha Waheshimiwa Wawakilishi kuwaunga mkono wananchi wao katika miradi midogo midogo wanayoianzisha kwa mujibu wa vipaumbele wanavyoviweka.
Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena, napenda niwakumbushe Waheshimiwa Wawakilishi kuwasilisha marejesho ya fedha walizopokea kwa mwaka 2012 kwa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais kwani hayo ni matakwa ya Sheria ambayo tumeijadili na kuipitisha kwa pamoja ndani ya Baraza letu hili. Haitokuwa jambo la busara kuja kuoneshana vidole humu ndani kwani sisi ni Viongozi na tunatakiwa tuwe mfano mzuri kwa jamii.  Kwa mujibu wa Sheria ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo ya mwaka 2013, Mheshimiwa Mwakilishi hatopatiwa fedha nyengine hadi atakapowasilisha marejesho kamili na sahihi.

MAMBO MUHIMU YALIYOJITOKEZA BARAZANI:
Mheshimiwa Spika, katika mkutano huu wa kumi na moja wa Baraza lako Tukufu, Serikali imewasilisha jumla ya Miswada mitano (5) ya Sheria ambayo inalenga kulinda ustawi na maslahi ya nchi yetu. Aidha, Baraza lako Tukufu lilipokea Ripoti za Utekelezaji wa Maagizo ya Kamati za Kudumu za Baraza kwa Wizara kwa mwaka 2011/2012 zilizowasilishwa na Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara husika. Pia, Baraza lilipokea Ripoti za Kamati za Kudumu za Baraza kwa mwaka 2012/2013 zilizowasilishwa na Wenyeviti wa Kamati hizo. Ripoti hizo zilijadiliwa na kuchangiwa kikamilifu na Waheshimiwa Wawakilishi.
Mheshimiwa Spika, vile vile, katika mkutano huu jumla ya maswali 82 ya msingi na maswali 167 ya nyongeza yaliulizwa na Waheshimiwa Wawakilishi na kujibiwa kwa ukamilifu na Waheshimiwa Mawaziri wa Wizara husika.
Mheshimiwa Spika, Mswada wa kwanza uliowasilishwa ulikuwa ni Mswada wa Sheria ya Kuanzisha Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma ya Maji na Nishati Zanzibar na Mambo Mengine Yanayohusiana na Hayo (ZURA).  Madhumuni ya Mswada huu ni kuanzisha Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati ambayo itasimamia ubora wa huduma inayotolewa kulingana na viwango pamoja na kudhibiti bei kwenye huduma za maji na nishati.
Katika kujadili Mswada huu, Kamati ya Mawasiliano na Ujenzi na Waheshimiwa Wajumbe kwa ujumla wao walisisitiza zaidi juu ya usimamizi na utoaji wa huduma bora za maji na nishati pamoja na kusimamia utolewaji wa leseni kwa wauzaji wa mafuta kwa kuzingatia viwango vilivyowekwa katika sheria hii. Napenda kuwahakikishia Waheshimiwa Wajumbe na wananchi kwa jumla kuwa Serikali imejidhatiti kuhakikisha kwamba huduma ya maji safi na salama na nishati itatolewa kwa kufuata misingi ya sheria hii ambayo itazingatia upatikanaji wa huduma bora, yenye viwango vinavyokubalika na itakayokidhi mahitaji ya watumiaji. Aidha, Mamlaka itasimamia viwango vya bei za maji na nishati ili kudhibiti upandaji wa bei hizo kiholela.
Mheshimiwa Spika, Mswada mwengine uliowasilishwa na kujadiliwa ni Mswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Shirika la Bandari na Mambo Mengine Yanayohusiana na Hayo. Mswada huu una madhumuni ya kufanya marekebisho ya Sheria ya Kuanzishwa kwa Shirika la Bandari Namba 1 ya Mwaka 1997 yenye lengo la kuweka mazingira bora ya uendeshaji na udhibiti wa Bandari pamoja na kukuza uwiano na mashirikiano mazuri kati ya Shirika na Mamlaka ya Usafiri wa Baharini.

Wakati wa kuujadili Mswada huo, Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu walishauri kuwepo na udhibiti na usimamizi mzuri wa uuzaji wa tiketi za kusafiria ili kudhibiti upakiaji wa idadi kubwa ya abiria kuliko uwezo wa vyombo hivyo. Aidha, suala la ujenzi wa gati lilichukua nafasi kubwa katika michango ya Waheshimiwa Wajumbe na walishauri kuwa Serikali ijenge bandari itakayokidhi mahitaji ya hivi sasa na baadae. Niwahakikishie Waheshimiwa Wajumbe kwamba Serikali inaendelea na jitihada za kuzungumza na Washirika wa Maendeleo ili kupata fedha kwa ajili ya kuliendeleza eneo la Mpiga Duri kwa kujenga bandari ya kisasa. Aidha, nachukua fursa hii kuzitaka Taasisi zote zinazohusika na usimamizi wa uuzwaji wa tiketi kuhakikisha kwamba suala la uuzwaji wa tiketi kiholela linadhibitiwa na kwamba yeyote atakaekwenda kinyume na sheria zilizopo achukuliwe hatua zinazofaa. Pia, niwaombe Waheshimiwa Wajumbe tushirikiane kuwaelimisha wananchi umuhimu wa kununua tiketi katika maeneo yaliyoruhusiwa ikiwa ni pamoja na kukataa kununua tiketi zinazouzwa kiholela mikononi mwa walanguzi kwa ajili ya kulinda usalama wao.
Mheshimiwa Spika, Mswada wa tatu uliowasilishwa na kujadiliwa na Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako ni Mswada wa Sheria ya Kuanzisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Kuweka Utekelezaji wa Majukumu na Uwezo na Mambo Mengine Yanayohusiana na Hayo. Wadhifa wa Mwanasheria Mkuu umeanzishwa na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha 55. Katika kifungu cha 56 cha Katiba hiyo, kinaeleza kazi za Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuwa ndiye atakayekuwa Mshauri Mkuu wa kisheria kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na atatekeleza shughuli nyengine zozote za kisheria zitazopelekwa kwake au atakazoagizwa na Rais au kwa mujibu wa Katiba hii au Sheria nyenginezo zozote. Kutokana na mapungufu ya kimsingi ambayo yanaathiri ufanisi wa utendaji kazi, Serikali imeona haja ya kuanzishwa kwa Sheria hii itakayoiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
Wakijadili mswada huu, Waheshimiwa Wajumbe waliishauri Serikali kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ishirikishwe kikamilifu katika kuandaa na kufunga mikataba mbali mbali ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa ili kuepuka watendaji kufunga mikataba mibovu. Serikali itaendelea kuitumia ipasavyo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa masuala yote yanayohusu sheria, ufungaji wa mikataba ambapo kitengo maalum cha kusimamia Mikataba kitaundwa ili kudhibiti mikataba na nyaraka za Serikali.

Mheshimiwa Spika, Mswada wa nne uliowasilishwa ni Mswada wa Sheria ya Mahkama ya Biashara Zanzibar na Mambo Mengine Yanayohusiana na Hayo. Madhumuni ya mswada huu ni kuanzisha mfumo madhubuti wa kufanya mageuzi na kuimarisha mfumo wa kisheria, kitaasisi na utendaji wa shughuli zake hapa Zanzibar. Pia mswada huu umezingatia changamoto zinazokabili utatuzi wa migogoro ya kibiashara hapa Zanzibar chini ya mfumo wa sheria uliopo sasa ambao unazingatia migogoro ya kibiashara kama migogoro mingine yeyote. Wakati wakichangia mswada huu Waheshimiwa Wajumbe walieleza kuwa kuna tatizo la kesi kukaa muda mrefu bila kusikilizwa na hivyo kuongeza malalamiko ya wadai na wadaiwa wa kesi hizo. Pia imeonekana kuwa kuna tatizo katika uwekaji wa kumbukumbu wa kesi zote zinazowasilishwa na zilizokamilika.
Mheshimiwa Spika, kupitia sheria hii Mahkama itaweka utaratibu mzuri kuhakikisha kuwa kesi zote zinazowasilishwa zinasikilizwa kwa muda mfupi zaidi. Aidha, suala la uwekaji wa kumbukumbu za kesi zote na utekelezaji wake litapatiwa ufumbuzi kwa kuanzishwa Daftari maalum la kumbukumbu ambalo litahifadhi kesi zote na maamuzi yanayotolewa.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza awali kwamba Baraza hili pia lilipokea na kujadili Ripoti za Utekelezaji wa Maagizo ya Kamati za Kudumu za Baraza kwa Wizara kwa mwaka 2011/2012 pamoja na Ripoti za Kamati za Kudumu za Baraza kwa mwaka 2012/2013. Waheshimiwa Mawaziri walitoa ufafanuzi wa kina na kwa ufasaha hoja zote zilizojitokeza. Nachukua nafasi hii kuwapongeza na kuwashukuru sana Wenyeviti wa Kamati na Wajumbe wao kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuishauri Serikali katika kutekeleza Majukumu yake ya kutoa huduma bora kwa wananchi. Aidha, napenda pia niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri kwa kutoa ufafanuzi wa hoja zote zilizotolewa na Waheshimiwa Wawakilishi, naamini hoja na ufafanuzi uliotolewa ni kwa lengo la kuimarisha utendaji wetu katika sekta mbali mbali za Serikali, ili Serikali yetu iendelee kuaminika mbele ya macho ya wananchi inaowatumikia.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza kwa dhati Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kwa namna walivyoichangia ripoti ya PAC kwa hisia kali zilizoonyesha utendaji dhaifu wa Watendaji wetu kwa matumzi yasiyoridhisha ya pesa za Serikali katika Mawizara na Taasisi mbali mbali za Serikali.  Nampongeza sana Mwenyekiti wa Kamati hii, Mheshimiwa Omar Ali Shehe pamoja na Wanakamati wake wote kwa kazi nzuri waliyoifanya ya kufanya uchunguzi wa kina kwenye Mawizara na Taasisi mbali mbali za Serikali mpaka wakaiwasilisha ripoti nzuri kama hii.
Mheshimiwa Spika, Mawaziri wakiwa wasimamizi wakuu wa watendaji wao wamezisikia hisia hizo na watafanya kila linalowezekana kuzirekebisha kasoro zilizoonekana. Ninaamini kuwa kasoro hizo zitarekebishwa na hazitorejewa tena.

Mheshimiwa Spika, katika michango iliyohusiana na Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati, liligusiwa suala la mafuta na gesi asilia kutolewa kutoka kwenye orodha ya Muungano, na wapi suala hili lilipofikia.
Mheshimiwa Spika, Kamati yetu inayoongozwa na Wanasheria Wakuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bado inalifanyia kazi suala hili.  Ninategemea tutapata taarifa ya awali ya namna suala hili linavyoendelea tutakapofanya kikao chetu cha pamoja kati ya SMT na SMZ chini ya Uenyekiti wa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuzungumzia kero (changamoto) za Muungano, kitakachofanyika tarehe 28 Aprili, 2013.  Lakini niseme tu Mheshimiwa Spika, kuwa suala hili si rahisi kama tulivyofikiria lina mambo mengi ya kiufundi ambayo ndiyo yanayofanyiwa kazi na Wanasheria Wakuu wa Serikali wa pande mbili.  Hata hivyo, nina matumaini makubwa kwamba Wanasheria wetu wakuu hawa, wa SMT na SMZ, watalifikisha jambo hili mahala pazuri katika muda mfupi utakaowezekana.
Mheshimiwa Spika, wakati wa kujadili ripoti ya Wizara ya Katiba na Sheria, baadhi ya Waheshimiwa Wajumbe waliitaka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itoe kauli yake kama Serikali ya kutoa mwongozo kuhusu suala la hatma ya Zanzibar katika suala zima la mjadala wa Katiba.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyokwishaeleza hapo awali, mchakato wa Katiba sasa unaingia katika hatua yake ya pili baada ya hapo zitabaki hatua za kufanyika kwa Bunge la Katiba kujadili rasimu ya Katiba hiyo na hatimae hatua ya kura ya maoni.
Mheshimiwa Spika, suala la mchakato wa Katiba linaendeshwa kwa kufuata sheria iliyotungwa kwa pamoja baina ya pande mbili za Muungano na kupitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na pia Baraza lako Tukufu.  Kwa hivyo, Mheshimiwa Spika, kutokana na mchakato kuendeshwa kwa kufuata sheria ambayo imeweka utaratibu mzima wa kuliendesha zoezi hilo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kama Serikali haina kauli ya kutoa mwongozo juu ya jambo hilo.  Tunaiachia Tume ya Katiba ifanye kazi yake.
Mheshimiwa Spika, katika hotuba yangu ya ufungaji wa kikao cha Baraza cha mwezi wa Januari, 2013 nililieleza Baraza lako Tukufu kuwa maandalizi  ya ununuzi wa meli ya abiria yameshakamilika, kilichosalia ni utiaji wa saini. Tumechelewa kukamilisha uwekaji wa saini mkataba wa kutengeneza meli hiyo, kutokana na kwamba tulitaka tujenga meli itakayokidhi haja yetu.  Meli hiyo itabeba abiria 1,200 pamoja na mizigo isiyopungua tani 200.  Aidha, meli hiyo itaweza kuhimili bahari yetu hasa mkondo wa Nungwi.
Mheshimiwa Spika,  sasa napenda kuliarifu Baraza lako Tukufu kuwa maandalizi yote juu ya ujenzi wa meli mpya ya abiria pamoja na mchoro wa meli yenyewe yamekamilika na fedha tulizozikusanya zitatumika kulipia sehemu ya gharama ya ujenzi wa meli hiyo na ni matarajio yangu kuwa utiwaji wa saini utakamilika ndani ya mwezi wa Mei, 2013.  Kadhalika, ujenzi wa meli hiyo unatarajiwa kuchukua miezi kumi na nane baada ya utiwaji wa saini.

HITIMISHO:
Mheshimiwa Spika, nachukua tena nafasi hii kukushukuru tena wewe binafsi kwa kuliendesha Baraza hili vizuri na kwa ufanisi wa hali ya juu. Pia nawashukuru Waheshimiwa Wawakilishi kwa kutekeleza Majukumu yao ya kuishauri Serikali na mwisho nawashukuru wananchi wote kufuatilia mwenendo wa Baraza letu hili.  Nawashukuru tena Waheshimiwa Wawakilishi wetu wa wananchi kwa michango yao ya uwazi ambayo ilikuwa na nia ya kuimarisha utendaji wa Serikali.  Nawapongeza sana Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu na tumepokea ushauri wao kwa mikono miwili.  Pamoja na kupokea mawazo, ushauri na mapendekezo yao na kuahidi kuyatekeleza, niseme tu pale ambapo Serikali imefanya vizuri basi nayo ipongezwe na kusifiwa ili kuitia moyo ifanye vizuri zaidi.
Mwisho, Mheshimiwa Spika, ninawatakia Waheshimiwa Wawakilishi kila la kheri na mafanikio mema katika kuwatumikia wananchi katika Majimbo yao na kuwatakia safari njema na salama ya kurejea Majimboni mwao.
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, sasa naomba kutoa hoja ya kuliakhirisha Baraza lako Tukufu hadi siku ya Jumatano, tarehe 12 Juni, 2013 saa 3.00 barabara za asubuhi.

Naomba kutoa hoja.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akisalimina na Baadhi ya Maafisa wa Ubalozi Mdogo wa China hapa Zanzibar waliohudhuria makabidhiano ya skuli rafiki kati ya China na Zanzibar iliyop[o Mwanakwerekwe ambayo imejengwa kwa msaada wa Serikali ya China.



 Balozi Mdogo wa China aliyepo Zanzibar Bibi Chen Qiiman na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakifungua pazoa kuashiria makabidhiano ya skuli mpya ya urafiki kati ya nchi hizo mbili iliyopo mtaa wa mwanakwerekwe.



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibarf Balozi Seif Ali Iddi akiangalia moja ya darasa liliomo ndani ya skuili mpya rafiki kati ya china na Zanzibar iliyopo mwanakwerekwe.



 Viwanja vya michezo mbali mbali vilivyomo ndani ya eneo la skuli mpya rafiki kati ya china na Zanzibar iliyopo mwanakwerekwe Wilaya ya Magharibi.



Balozi Mdogo wa China aliyepo Zanzibar Bibi Chen Qiiman na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Mh. Ali Juma Shamhuna wakitia saini mkataba wa makabidhiano ya skuli mpya rafiki kati ya China na Zanzibar hapo ilipo skuli hiyo Mwanakwerekwe.





 Baadhi ya Maafisa wa Ubalozi Mdogo wa China na familia zao wakishuhudia hafla ya makabidhiano ya skuli mpya rafiki kati ya china na Zanzibar iliyojengwa kwa msaada wa Serikal;I ya China hapo Mwanakwerekwe wilaya ya Magharibi.



 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar balozi Seif Ali Iddi akiwa katika picha ya pamoja na Viongozi  mbali mbali waliohudhuria hafla maalum ya makabidhiano ya skuli mpya ya urafiki kati ya China na Zanzibar mara baada ya makabidhiano hayo.
Picha na Hassan Issa wa – OMPR – ZNZ .




Mlezi wa Soko la Jumapili { Sunday Market }ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akinunua bidhaa mbali mbali zilizotengenezwa na wajasiri amali wa soko hilo hapo Kisonge Michenzani.




Balozi Seif akizungumza na Katibu wa Wajasiri amali wa soko la Jumapili { Sunday Market }  Bibi Mtumwa Ali Juma hapo Kisonge Michenzani mara baada ya kuwatembelea kuona shughuli zao.







 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Vijana wa Baraza ya City Centre iliyopo Kisonge Michenzani na kuwaasa wajiunge pamoja ili kupata nguvu ya kunzisha miradi itakayowasaidia kimaisha.
Picha no Hassan Issa wa –OMPR – ZNZ.





Friday, 19 April 2013


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa katika dua ya pamoja na kutakia malazi mema Gwiji la sanaa Zanzibar Bi Ftma Binti Baraka { Bi Kidude } hapo nyumbani kwake Rahaelo nyuma ya Studio ya ZBC Redio.Kulia ya Balozi Ni mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mjini Nd. Borafia Mtumwa na Kushoto yake ni Mwakilishi wa Jimbo la Rahaleo Mh. Nassor Al – Jazira.


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa pamoja na baadhi ya Familia ya Bi Kidude wakati alipofika kutoa mkono wa pole kwa ndugu na jamaa wa msanii huyo.Kushotoya Balozi  ni Nd. Haji Ramadhani Suwed na kulia ni Bwana Abdullrahman Saleh



Umati mkubwa wa Wananchi walioshiriki mazishi ya Msanii Gwiji wa sanaa kanda ya Afrika Mashariki na Mipaka yake Bibib Fatma Binti Baraka { Bi Kidude } hapo nyumbani kwake Rahaleo nyuma ya Studio ya ZBC Redio.
Picha no:- 091 ni:- Baadhi ya waumini wa Dini ya Kiislamu wakendelea na dua ya kumtakia safari njema msanii Gwiji wa Taarab Bi Fatma Binti Baraka { Bi Kidude } hapo nyumbani kwake 



Shamrashamra za ufunguzi wa nyumba ya walimu Mzuri kaja, Makunduchi