Tuesday, 1 October 2013

 Mmoja kati ya Wakulima wa Kijiji cha Nguruweni Dole Mzee Kitwana Mustaha aliishukuru na Kuipongeza  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif  Ali Iddi kwa kukamilisha ahadi yake ya kuwapatia hati za umiliki wa mashamba  wakulima hao kwa ajili ya kilimo katika maeneo yaliyowahi kuleta mgogoro kwa muda mrefu.
 Baadhi ya wananchi na wakulima wa Kijiji cha Nguruweni wakiwa katika mkutano maalum  uliotishwa  na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif wa kukabidhiwa hati za umiliki wa mashamba ya kilimo katika maeneo yao.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akizungumza na wakulima wa Kijiji cha Nguruweni kabla ya kuwakabidhi hati za umiliki wa mashamba ya kilimo wakulima hao.
 Balozi Seif Ali Iddi akimkabidhi Hati ya umiliki wa shamba Bibi Josephine Yohana kwenye hafla maalum ya kumaliza mgogoro wa mashamba katika kijiji hicho.
 Balozi Seif akimpatia Hati Bwana Mohd Ali Pili ya kumiliki eneo la kilimo katika Kijiji cha Nguruweni  ambako kuliibuka mgogoro uliosababishwa na kuinbgizwa watu wasiohusika na maeneo hayo kwa kilimo.
























Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imewatahadharisha Wakulima wa Viijiji vya Ndunduke, Nguruweni na Dole  kuhakikisha kwamba maeneo ya kilimo waliyokabidhiwa na Serikali kwa shughuli za Kilimo wanayatumia  kama yalivyopangwa na kukubalika na pande hizo mbili.
Wakulima hao wakaonywa kuwa  ye yote atakaeamua maeneo hayo kuyakata viwanja kwa ajili ya kujenga nyumba au kuyauza kwa mtu mwengine aelewe kwamba Serikali italazimika kumnyang’anya mkulima huyo mara moja.
Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati akikabidhi hati  za umiliki wa mashamba ya kilimo kwa ajili ya wakulima 40 kati ya 181 wa Kijiji cha Nguruweni waliokuwa wakiilalamikia Serikali kwa kipindi kirefu kuidhinishiwa  mashamba wanayoyatumia ili kuendeleza shughuli zao za Kilimo.
Balozi Seif alisema wapo baadhi ya watu wenye tabia ya kuomba mashamba au eka kwa kisingizio cha kuendeleza kilimo lakini badala yake hujenga  tamaa inayowaelekeza kuanza kukata viwanja na kuuzia watu wengine.
“ Nataka nitahadharishe kabisa kwamba Mkulima ye yote atakayediriki kutumia fursa aliyopewa na Serikali ya kuendeleza kilimo kwenye shamba alilokabidhiwa na akaamua kufanya vyengine afahamu kwamba Serikali haitasita kunyang’anya shamba hilo mara moja “. Alitahadharisha Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif  aliwapongeza wakulima hao wa Nguruweni kwa ustahamilivu wao mkubwa waliouchukuwa kwa kipindi kirefu kufuatia mgogoro wa maeneo waliyokuwa wakitumia kwa shughuli za kilimo baadhi yake kupewa watu wengine.
Balozi Seif alisema ustahamilivu huo kwa kiasi kikubwa umesaidia kuendeleza amani na utulivu kwenye Vijijini hivyo vya Nguruweni, Ndunduke pamoja  na Dole ambayo imeleta faraja kwa Serikali Kuu kwa vile haikuathiri shughuli za kila siku za kijamii.
Aliwakumbusha wakulima hao kwamba hivi sasa ni muda muwafaka wa kuendeleza shughuli zao za kilimo kwa vile wameshakuwa na uhalali wa kufanya hivyo katika maeneo waliyopewa na Serikali.
Alifahamisha kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikisisitiza na kuhimiza kilimo kwa vile sekta hiyo bado inaendelea kuwa muhimili Mkuu wa uchumi wa Taifa hili.
“ Serikali imekuwa ikihimiza na kusisitiza umuhimu wa kilimo. Lakini Mkulima hawezi kuendeleza kilimo bila ya kuwa eneo la kilimo, sasa kwenu nyinyi hili suala  linaonekana kuondoka “. Alifafanua Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimpongeza Mwenyekiti wa Kamati Maalum aliyoiunda kushughulikia mgogoro huo wa mashamba ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mh. Abdulla Mwinyi kwa kushirikiana vyema na watendaji wa Wizara za Kilimo na Ardhi na kuutatua mgogoro huo wa muda mrefu.
Mapema Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo na Mali Asili Nd. Ali Juma alisema Taasisi za Kilimo na Ardhi zililazimika kufanya uhakiki wa kina ili kuwatambua wakulima halali waliokuwa wakistahiki kupatiwa hati hizo.
Nd. Ali alisema uhakiki huo ulioshirikisha pia Masheha wa Vijiji vilivyohusika na mgogoro huo vya Nguruweni Ndunduke na Dole umeibua wakulima wapatao 181 ambapo  wakulima 40 kati ya hao wamethibitika kupatiwa hati hizo kwa awamu ya kwanza.
Naibu Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Kilimo na Mali Asili alieleza kwamba kazi ya uhakiki sambamba na uchambuzi kwa wakulima wa Kijiji cha Dole imeshaanza rasmi na inatarajiwa kukamilika katika kipindi kifupi kijacho.
Akitoa shukrani zake Mwenyekiti wa Kamati  Maalum iliyounda  na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Balozib Seif kushughulikia mgogoro huo wa mashamba ya vijiji vya Nguruweni, Ndunduke na Dole Mh. Abdulla Mwinyi  alisema Wakulima wa Vijiji hivyo  wanapaswa kupongezwa kwa umahiri wao wa ustahamilivu kufuatia mgogoro huo wa mashamba kwenye eneo hilo.
Hata hivyo Mh. Abdulla Mwinyi ambae pia ni Mkuu wa Mkoa Mjini Magharibi amewaomba wale wakulima ambao bado mgogoro wao haujapatiwa ufumbuzi waendelee kuwa na subra kwa vile Serikali kupitia Uongozi wa Kamati hiyo unajitahidi katika kukamilisha mchakato huo.
Akitoa shukrani kwa Niaba ya Wakulima hao Mmoja wa Wazee wa Vijiji hivyo Mzee Kitwana  Mustafa alimpongeza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kwa ujasiri na uungwana wake aliouchukuwa wa kutimiza ahadi aliyowapa  mwaka jana wa kumalizika kwa kadia hiyo.
Mzee Kitwana alisema wakulima wa Vijiji hivyo wamefarajika na hatua iliyochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwatatulia kero lililokuwa likiwasumbua kwa miaka mingi iliyopita.
“ Ile furaha yetu tuliyonayo leo kama tumengeruhusiwa basi tunatamani tukubebe na matope yetu Mzee wetu kwa jinsi ulivyotujali na kututhamini  kwa katambua kwamba tulikuwa tukisumbuka kweli kweli “ Alionyesha furaha yake Mzee Kitwana.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliwahi kutoa  ahadi kwa wakulima hao wa Nguruweni, Ndunduke na Dole  kwamba Serikali  itayagawa maeneo  yote ambayo kamati aliyoiunda tarehe 14 Disemba Mwaka 2012 Chini ya Mwenyekiti wake Mh. Abdulla Mwinyi  kufanya uhakiki wa mashamba yote yaliyoleta mgogoro.
Wakulima hao waliwahi kutoa shutuma kali kwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Balozi Seif dhidi ya watendaji na Maafisa  wanaosimamia Ardhi, Kilimo wakiwemo pia Viongozi wa ngazi ya kati wa Serikali kwa vitendo vyao vya kuingiza wakulima waliokuwa hawahusiki na mashamba hayo.
Watendaji hao walituhumiwa na wakulima hao kuvuruga  jukumu  walilopewa la kusimamia maandalizi ya utolewaji wa nyaraka kwa wakulima 28 wa awamu ya kwanza waliokubalika kupatiwa hati za umiliki huo chini ya aliyekuwa waziri Kiongozi wa mwisho wa SMZ  Mh. Shamsi Vuai Nahodha.
 Serikali ililazimika kuzuia utolewaji wa hati hizo kufuatia hitilafu zilizojichomoza za kupandikizwa baadhi ya watu wasiohusika jambo ambalo lilisababisha mgogoro wa muda mrefu kati ya wakulima hao na watendaji waliopewa jukumu la kusimamia suala hilo.

 Othman Khamis  Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
1/10/2013.

Wednesday, 18 September 2013

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akitembelea maendeleo ya uzalishaji wa umeme kupitia miundo mbinu iliyopo hivi sasa kwenye kituo kikuu cha umeme Mtoni.

  Kaimu Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme Zanzibar { ZECO} Thabit Salum Khamis akimuelezea Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif  mfumo mpya wa huduma za umeme unaotumika katika kituo kikuu cha Umeme kilichopo Mtoni wakati alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya huduma za umeme Nchini.

 Mhandisi  wa Vituo vya Umeme katika shirika la Umeme Zanzibar { ZECO } Mohd Juma Othman akimfafanulia  Balozi Seif mfumo wa ugawaji wa laini za umeme mkubwa kwenda katika vituo vipya vilivyojengwa kwa lengo la kutoa huduma za uhakika za Umeme maeneo tofauti Nchini.

 Mhandisi  wa Vituo vya Umeme katika shirika la Umeme Zanzibar { ZECO } Mohd Juma Othman akimfafanulia  Balozi Seif mfumo wa ugawaji wa laini za umeme mkubwa kwenda katika vituo vipya vilivyojengwa kwa lengo la kutoa huduma za uhakika za Umeme maeneo tofauti Nchini.

Mhandisi  wa Vituo vya Umeme katika shirika la Umeme Zanzibar { ZECO } Mohd Juma Othman akimfafanulia  Balozi Seif mfumo wa ugawaji wa laini za umeme mkubwa kwenda katika vituo vipya vilivyojengwa kwa lengo la kutoa huduma za uhakika za Umeme maeneo tofauti Nchini.

 Press Release

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji Nishati na Madini imeombwa kufikiria njia muwafaka ya kuyauza Majanareta yaliyopo katika kituo kikuu cha kupokelea Umeme Mtoni ili kuwepusha hasara endapo yataendelea kuwepo eneo hilo bila ya matumizi.
Majanareta hayo 30 yalikuwa yakitoa huduma za umeme wa dharura katika kipindi ambacho Zanzibar ilikuwa ikikabiliwa na uhaba mkubwa wa huduma ya nishati ya umeme kutokana na kinanzio chake ilichokuwa ikikitumia wakati huo kutokidhi mahitaji halisi ya huduma hiyo Nchini.
Mhandisi wa Maganareta katika Kituo Kikuu cha Umeme Mtoni Yussuf Reja alitoa ushauri huo wakati wa ziara ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kuangalia maendeleo ya uzalishaji wa huduma ya umeme Nchini kupitia miundo mbinu iliyopo katika kituo hicho.
Mhandisi Yussuf Reja alimueleza Balozi Seif kwamba Majanareta hayo yako katika kiwango  bora lakini tatizo kubwa liliopo ni huduma ya mafuta ambayo ni maalum { IDO } na yana  hitaji  gharama kubwa za uendeshaji.
Alisema Shirika la Umeme lilikuwa likipata hasara ya zaidi ya shilingi Milioni 16,000,000/-  kwa saa wakati maganareta hayo yalipokuwa yakiwashwa kusaidia huduma za umeme katika kipindi cha mgao wa huduma hiyo muhimu.
Mhandisi Yussuf Reja alifahamisha kwamba shirika la umeme lilikuwa likizalisha umeme kupitia Maganareta hayo kwa  uniti moja yenye  thamani ya shilingi 500/-  ambayo ingelazimika kuwauzia wateja wake uniti moja kwa shilingi 700/- gharama ambayo ni mzigo kwa mwananchi wa kawaida.
“ Ukweli uliowazi gharama ya kuyaendesha Maganareta hayo kupitia shirika la Umeme ni kubwa mno na inaweza kuleta maafa kwa shirika hilo endapo yataendelea kutumiwa “. Alitahadharisha Mhandisi Yussuf Reja.
Naye Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji, Nishati na Madini Nd.Mustafa Aboud Jumbe alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Wizara hiyo tayari imeshapokea mapendekezo ya Shirika hilo kuhusiana na majanareta hayo ya Kituo cha Umeme Mtoni.
Naibu Katibu Mkuu huyo wa Ardhi  Mustafa Jumbe alisema Wizara hiyo inajipanga kuyafanyia kazi mapendekezo hayo na baadaye kuyawasilisha Serikali kuu kwa ajili ya kupatia ufumbuzi muwafaka.
Mapema Kaimu Meneja Mkuu wa Shirika la Umeme Zanzibar { ZECO } Thabit Salum Khamis alisema mfumo mpya wa kisasa wa huduma za umeme kwenye kituo kikuu cha Umeme Mtoni uitwao { SCADA } umewawezesha watendaji wa shirika hilo kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa.
Thabit Salum alimfahamisha Balozi Seif kwamba mfumo huo umepunguza kero kubwa ya kukatika katika kwa umeme kulikokuwa kukitoa usumbufu kwa wananchi walio wengi kwenye maeneo mbali mbali wakati inapotokea hitilafu.
Alieleza kwamba shirika la umeme limekuwa na vituo vikubwa vinavyosambaza umeme kutoka kituo kikuu cha Mtoni kwenda Welezo na Fumba ambavyo vimepangwa kusambaza huduma hiyo na kuacha mfumo wa zamani wa kutumia laini moja tuu.
Kaimu Meneja huyo wa Shirika la Umeme aliongeza kwamba matumizi zaidi ya  umeme huongezeka kutoka Mega walts 33.16 nyakati za asubuhi hadi kufikia  Mega Walts 48.1 kipindi cha  jioni lakini huduma hiyo kuongezeka zaidi katika kipindi cha siku kuu na kufikia hadi Mega Walts 52.
Uwezo wa laini mpya ya umeme uliopo Zanzibar hivi sasa imefikia Mega Walts mia moja  ambapo shirika limekuwa na hakiba ya umeme kwa zaidi ya asilimia 50% mbali ya ile laini ya zamani yenye uwezo wa mega walts 40 kutokana na kuchakaa kwake.
Akitoa nasaha zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliwatanabahisha watendaji wa shirika la umeme kwamba huduma ya umeme hivi sasa imekuwa nyenzo  muhimu ya kiuchumi kwa vile inasaidia kipato cha mwananchi.
Balozi Seif alisema ni vyema kwa watendaji wa shirika la umeme kufanya kazi zao katika mazingira ya ushindani mfano wa kuwepo  mashirika mengine yanayotoa huduma hizo hapa nchini kwa lengo la kupata ufanisi sambamba na kutoa huduma bora kwa wateja wake.
“ Watendaji lazima mfanye kazi kama mko katika ushindani wa kibiashara  na mashirika mengine licha ya kwamba mpo peke yenu. Kila mkiamka lazima mfikirie mtaongeza vipi wateja wengine wapya “. Alisisitiza Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwakumbusha wafanyakazi wa shirika hilo kuendelea kuwaelimisha wananchi juu ya athari na hatari ya kutumia mafundi wa mitaani katika kuungiwa huduma hiyo jambo ambalo mara nyingi huleta hasara kutokana na hitilafu zinazojitokeza baadaye.

Monday, 16 September 2013

Balozi Seif Ali Iddi alipofanya ziara fupi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Tawi la Chama cha Mapinduzi la Kijiji cha Kiomba Mvua

 Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif Ali Iddi akikagua maendeleo ya Ujenzi wa Tawi Jipya la CCM la Kiomba Mvua akiongozana na Mwenyekiti wa Tawi hilo Bibi Zawadi Ali Suleiman.

 Mjumbe wa Kamati Kuu yaHalmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Balozi Seif  akikabidhi vifaa kwa ajili ya uendelezaji wa  ujenzi wa Tawi la CCM Kiomba Mvua kwa Mwenyekiti wa Tawi hilo Zawadi Ali Suleiman wakati alipofanya ziafa fupi ya kukagua maendeleo ya ujenzi huo.

 Mbunge wa Jimbo la Kitope Balozi Seif  Ali iddi akimkabidhi mchango wa fedha Mwakilishi wa Kikundi cha Polisi Jamii cha Kijiji cha Kitope Nd. Bakari Khamis Simai pamoja na ahadi ya fulana kwa ajili ya kikundi chao cha ulinzi.
























Balozi Seif akimkabidhi mchango wa fedha mwakilishi wa Kikundi cha Polisi Jamii cha Kijiji cha Mbaleni Nd. Haji Shaali pamoja na ahadi ya fulana ili kuimarisha ulinzi katika kijiji hicho.

 Press Release:-
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi Balozi Seif Ali Iddi alisema Viongozi na Wanachama wa CCM wanapaswa  kuendelea kufanya vikao vyao kwa mujibu wa Kanuni na Taratibu za Chama hicho ili kuwa na uhalali kamili wa maamuzi wanayoyatoa kuhusu chama chao.
Kauli hiyo aliitoa wakati alipofanya ziara fupi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa Tawi la Chama cha Mapinduzi  la Kijiji cha Kiomba Mvua na baadaye kukabidhi  vifaa mbali mbali vya uendelezaji ujenzi wa Tawi hilo.
Vifaa alivyokabidhi  Balozi Seif ambaye pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar na Mbunge wa Jimbo la Kitope ni pamoja na Mabati, saruji, mchanga kokoto, nondo, mbao pamoja miti kwa ajili ya ukamilishaji wa Tawi jipya la Kijiji hicho.
Hafla hiyo ilikwenda sambamba na Vikundi vya Polisi jamii vya Kijiji cha Kitope na Mbaleni kukabidhiwa Fedha taslimu na ahadi za fulana kwa ajili ya kuimarisha kazi za za ulinzi, mchango na vifaa vyote hivyo vikigharimu jumla ya Shilingi Milioni 4,000,000/-
Balozi Seif alisema maamuzi ya chama kwa mujibu wa kanuni za CCM hutakiwa kufanyika ndani ya vikao halali vya Viongozi na wanachama wenyewe jambo ambalo husaidia kuepusha minong’ono na hata majungu miongoni mwa wanachama wa chama hicho.
Alitahadharisha kwamba maamuzi ya chama hayatolewi bara barani na ndio maana Katiba ya CCM ikasisitiza kujengwa Ofisi bora za chama hicho   na zenye kwenda na wakati  zinazolingana na hadhi ya chama ili wana chama hao wapate fursa nzuri ya kutoa maamuzi kwenye ofisi zao.
Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi aliwapongeza wana CCM wa Tawi hilo kwa uamuzi wao wa kujenga Tawi Jipya na la Kisasa likiwa pia na sehemu ya miradi ya  kiuchumi.
“ Chama cha Mapinduzi katika ngazi zake zote lazima kiwe na miradi ya kiuchumi itakayosaidia utekelezaji wa kazi  za chama hicho katika ngazi husika ili kujilinda na utegemezi kutoka ngazi za juu za chama  “. Alisisitiza Balozi Seif.
Alifahamisha kwamba uwamuzi wao huo ni sahihi na unakwenda sambamba na lengo la Chama ndani ya Jimbo la Kitope la kuwa na Ofisi mpya za kisasa zinazokwenda na wakati
Alieleza faraja yake kuona kwamba Jimbo la Kitope katika Matawi yake 20 hadi sasa tayari Ofisi 16 za chama cha Mapinduzi zimeshakamilika kujengwa majengo mapya ikibakisha Matawi manne tu.


Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
13/9/2013.

Tuesday, 10 September 2013

KUMBUKUMBU YA WALIOFAKI KWA MELI --ZANZIBAR

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imesema inaendelea na hatua mbali mbali za kujipanga katika sekta ya usafiri wa baharini ili kuepusha ajali ya meli kuzama isitokee tena  kama ilivyotokea ajali ya Mv.Skagit na MV.Spice islander.

Hayo wameelezwa na Waziri wa Fedha Zanzibar,Mhe.Omar Yussuf Mzee katika kikao cha kumbukumbu ya wahanga walifarika katika ajali hiyo kilichaandaliwa na waandishi wa habari wa maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA).

Alisema Serikali ilichukua juhudi za kuchunguza na kubaini makosa mengi,ambayo yamesababisha ajali ya meli hizo kuzama,hivyo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar  imepanga mikati mengi ya kuzuia ajali kama hiyo isitokee tena nchini.

Alisema Serikali ilibaini baadhi ya meli zilifanyiwa maarifa ya kuongezwa ukubwa (Modefication) hivyo Serikali imezisimamisha meli hizo kuendelea kutoa huduma ya usafiri wa baharini.

Mzee alisema Serikali  ilibani kulikua na meli zilikuwa zinafanyakazi kinyume na usajili wake,baada ya kubeba mizigo ilikua na beba abiria,ikiwemo tatizo kuajiri wafanyakazi wasiokuwa na sifa ya utaalam wa kazi hizo.Pia alisema baadhi ya meli zilikua hazina vifaa vya kujihami(life Jacket).

Alisema kutokana msiba mkubwa uliotokea wa Meli hizo mbili kuzama Mv.Skagit na MV.Spice Ilander  Mhe.Rais wa Zanzibar Dkt Ali Mohamed Shein ameagiza Serikali ichukua hatua ya ununuzi wa meli mpya ya abiria na mizingo.

Alisema katika maagizo ya Mhe.Rais Dkt Shein ameagiza ijengwe meli yenye ubora na yenye usalama ambapo  hatua  za ujenzi wa meli mpya ya abiria imeshaanza kujengwa nchini Korea ya Kusini.

Alielezea Meli hiyo mpya itakuwa na mashini mbili(Engine) ikiwemo na rada,chumba  ambacho kitaweza kufifadhi maiti wa wawili pamoja na chumba cha Daktari atakaekuwa yumo ndani ya meli kila itakapokuwa ipo safarini.

Aidha Mzee alisema Serikali haikukaa kimya imezitaka wamiliki wa vyombo vya usafiri wa baharini vyote viwe na bima ilikua hai(LIVE).Pia alisema Serikali imeshatoa amri meli itakayopakia abiria zaidi  ya uwezo wake isiondoke kinyume na agizo hilo captain na mkuu wa bandari wote watafikishwa katika vyombo vya sheria.

Kwa upande wa wajumbe wa Kikao akizunguza bibi mzuri aliiomba Serikali kuwafikiria jinsi ya kuwasaidia watu walioathirika kisaikolojia kutokana na ajali za meli hizo kuzama.
Alisema kuna watu wameathirika kisaikolojia kwa kupoteza watoto wane kwa wakati mmoja ,baadhi ya wanawake kupoteza mume na watoto.

Kikao hicho kimeandaliwa na Jumuia ya waandishi wa habri za maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA)  ikiwa ni siku ya kumbukumbu ya kuwakumbuka wahanga waliofariki katika ajali ya meli ya Mv.Skagit na Mv.Spice islander iliotokea Septemba 2011 na Julai 2012.
 




Monday, 9 September 2013








Hatimae Mabingwa wa Mashindano ya Ujirani mwema ya Dr. Sheni Cup yaliyoandaliwa na Umoja wa Vijana wa CCM Jimbo la Nungwi na kufadhiliwa na Rais wa Zanzibar Dr. Ali  Mohammed Sheni amepatikana katika mchezo wa Fainali ya mashindano hayo yaliyozikutanisha Timu za Soka za Kitamli ya Nungwi  dhidi ya wapinzani wao Timu ya Soka ya Mwendo Mdundo ya Kidoti.
Pambano hilo la Fainali lililoshuhudiwa na umati mkubwa wa wapenzi wa soka wa Jimbo la Nungwi na Vitongoji vyake limeiwezesha Wenyeji wa mashindano hayo Timu ya Kitamli ya Nungwi kuibuka na ushindi kwa kuilaza Mwendo Mdundo ya Kidoti Goli 1-0.
Timu ya Kitamli ilijipatia goli lake la pekee na la ushindi lililofungwa na mchezaji Haji Wa Haji katika kipindi cha kwanza cha mchezo huo  ambapo mgeni rasmi katika pambano hilo la Fainali ya Dr. Sheni Cup alikuwa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.
Mashindano hayo ya ujirani mwema  yaliyoanza kutimua vumbi Tarehe 24/8/2013 yamejumuisha Timu  Tisa kutoka katika vijiji tofauti vya Jimbo la Nungwi yakienda sambamba na yale ya mchezo wa Pete { Net Ball } kwa Wanawake yaliyojumuisha Timu Nne.
Akizungumza mara baada ya pambano hilo la Fainali Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliwahimiza Vijana hao kujitahidi kujifunza zaidi michezo ili wajijengee njia rahisi ya kupata ajira kupitia sekta ya michezo ambayo wakati huu imekuwa na thamani kubwa Duniani.
Balozi Seif alisema Ulimwengu hivi sasa umeshuhudia ongezeko kubwa la ajira kupitia Sekta ya michezo hasa Mchezo wa soka na Table Tennis ambayo imeonekana kutajirisha wanamichezo wengi wenye vipaji vikubwa vya michezo hiyo.
“ Tumeshuhudia wachezaji mbali mbali Duniani wakiwemo pia wale wanaotokea Bara letu la Afrika wakicheza mpira wa kulipwa katika timu mbali mbali za bara la Ulaya hasa ndani ya Uingereza. Huo ni Mfano halisi mmaopaswa kuutilia maanani ili na nyinyi siku moja mjikute mmetinga katika vilabu hivyo maarufu Duniani “. Alisisitiza Balozi Seif.
Mapema Mlezi wa Jimbo la Numngwi ambae pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum Haji Omar Kheir alisema mashindano hayo yaliyoandaliwa na Umoja wa Vijana wa CCM wa Jimbo hilo kwa  ushauri wa Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mama Asha Suleiman Iddi ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2010.
Haji Omar alisema ilani hiyo imeeleza umuhimu wa uimarisha michezo katika maeneo mbali mbali nchini   lengo likiwa  kuwajengea afya njema pamoja na ajira wananchi wanaoshiriki michezo hiyo.
Katika kuunga mkono uendelevu wa mashindano hayo Waziri Haji Omar aliahidi kuchukuwa dhamana ya malipo kwa deni linalodaiwa Kamati ya mashindano hayo linalohusu malipo ya posho za waamuzi pamoja na baadhi ya vifaa vya mashindano hayo.
Katika fainali hiyo  Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikabidhi Kikombe kwa Mabingwa wa Mashindano hayo Timu ya Kitamli ya Nungwi, Jezi, Mpira pamoja na Shilingi laki 300,000/-.
Balozi Seif pia alimkabidhi mshindi wa pili Mwendo Mdundo ya Kidoti Jezi, Mpira na Shilingi Laki 150,000/- wakati mshindi wa Tatu Timu ya Mapinduzi ya Kidagoni ikakabidhiwa  Jezi, Mpira na Shilingi 75,000/-.
Baadae Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akakabidhi shilingi 50,000/- kwa kila Timu bora , Mchezaji bora, mfungaji bora, Muamuzi bora, Mchezaji mdogo kuliko wote,kipa bora  pamoja na kocha bora kwenye mashindano hayo.
 Mashindano hayo yaliyopewa jina la Dr. Sheni Cup kwa mchezo wa Soka na Mwanamwema Sheni Cup kwa mchezo wa Pete { Net Ball } yamegharimu jumla ya shilingi milioni Sita Nukta Tano { 6,500,000/- }.
Wakati huo huo Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikabidhi mchango wa shilingi Milioni 2,000,000/- kwa ajili ya kusaidia ufufuaji wa michezo ya ndani { Indo games } hapa Nchini ambayo mingi inaonekana kufifia na mengije kufa kabisa kwa  kipindi kirefu sasa.
Akikabidhi mchango huo kwa Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar  { BTMZ } Sharifa Khamis hapo Ofisini kwake vuga Mjini Zanzibar Balozi Seif alisema Zanzibar ilikuwa ikisifika kimataifa kwa michezo ya ndani sifa ambayo hivi sasa imekufa kutokana na kufifia kwa michezo hiyo.
Alisema juhudi za pamoja zinahitajika kuchukuliwa katika kuona michezo hiyo inachipuka tena hapa Nchini kwa kuwapa nguvu za uwezeshaji na vifaa wachezaji wanaojihusisha na  michezo hiyo.
“ Vijana lazima waendeleze pia michezo ya ndani kama vile Table Tennis, Vinyoya, Beach Ball, Triatholon na riadha badala ya kuelekezaa  nguvu zao zaidi kwenye soka ili kurejesha sifa hiyo Kimataifa “. Alisisitiza Balozi Seif.
Akipokea mchango huo Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar             { BTMZ } Sharifa Khamis { Sherry } alisema msaada huo wa Balozi Seif ni hatua ya awali katika kuunga mkono juhudi zinazochukuliwa na Taasisi za Michezo Nchini katika kufufua vuguvugu la michezo hapa Nchini.
Mwenyekiti Sharifa { Sherry } alisema katika kwenda samba mba na ufufuaji huo Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar kwa kushirikiana na Chama cha Soka Zanzibar        { ZFA } hivi karibuni  vinatarajiwa kufungua vuguvugu la michezo katika kutimia miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
 9/9/2013.



Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuanzisha Wizara inayosimamia  sekta  ya kazi  ni  kuhakikisha kwamba inapambana na tatizo  la ajira linaloonekana kuathiri nguvu kubwa ya Vijana hapa Nchini.
Kauli hiyo aliitoa wakati  akizindua rasmi  Chuo cha Ushoni cha ujasiri amali  kilichoanzishwa na  Jumuiya ya Vijana ya Kibweni { Kibweni Yourth Organization } kiliopo katika Mtaa wa Kwa Botoro Kibweni ndani ya Jimbo la Bububu.
Balozi Seif alisema hatua hiyo ya Serikali inakwenda samba mba na utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2010 inayoelezea umuhimu wa kuundwa  kwa vikundi vya  ujasiri amali ambavyo hutoa fursa kubwa ya ajira miongoni mwa wananchi.
Alisema kazi za ujasiri amali zimekuwa zikisaidia kupunguza umaskini  na Serikali itajitahidi kuhakikisha inavijengea nguvu vikundi hivyo vya Jamii ili viweze kutekeleza majumu iliyojipangia.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliipongeza Jumuiya ya Vijana ya Kibweni kwa uamuzi wake wa kuanzisha Kikundi hicho ambacho ni mkombozi kwa wanajumuiya pamoja na vijana wa Jimbo hilo.
Hata hivyo Balozi Seif alihimiza viongozi na wana jumuiya hiyo kuwa wastahamilivu na kuvumiliana katika harakati zao za kila siku na hatua hiyo aliielezea kwamba itafanikiwa endapo utaratibu wa kufuata kanuni walizojiwekea utazingatiwa zaidi.
“ Nimefurahi kuona Vijana mmejikusanya kuanzisha mfumo wa ajira ambao Serikali kuu kadri ya hali itakavyoruhusu itazingatia na kutoa msaada unaostahiki ili kukiendeleza kikundi chenu “. Alisisitiza Balozi Seif.
Alihimiza mpango wa kuendelea kupanda miti ulionzishwa na vijana hao wa Kibweni ili kukabiliana na upungufu wa maji uliyoikumba nchi kutokana na tabia za baadhi ya watu kukata miti ovyo.
Katika kuunga mkono juhudi za Vijana hao wa Kibweni za kuanzisha Chuo cha Ushoni cha ujasiri amali Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif alikabidhi Vyarahani vitano kama mchango wake wa kukipa nguvu Chuo hicho.
Balozi Seif pia aliahidi kuchangia Kompyuta moja na Mashine ya Kudarzi kwa chuo hicho hatua  ambayo imeungwa Mkono na Mwakilishi wa jimbo la Bububu Hussein Ibrahim Makungu aliyetoa mchango wa Shilingi Milioni 2,000,000/- taslim wakati Mbunge wa Jimbo hilo Masoud Sururu ambae ndie mlezi wa Jumuiya hiyo akaahidi kuchangia Vyarahani Vitano, Pasi na Vifaa vidogo vidogo.
Akisoma  Risala ya wanajumiya hiyo ya Vijana wa Kibweni  mmoja wa mwanachama wa Jumuiya hiyo Farida Juma Haji alisema Vijana wa Kibweni wameamua kuanzisha  jumuiya hiyo wakitambua kwamba Serikali Kuu haina fursa ya kutoa ajira kwa watu wote.
Alisema elimu ya ujasiri amali ambayo ni muhimu kwa taifa lolote Duniani ndio itakayowapa nafasi pekee ya kukabiliana na tatizo hilo la ajira na upande mwengine jumuiya imelenga kwenda sambamba na mpango wa Taifa wa kupunguza Umaskini Zanzibar { Mkuza }.
Mapema akikikagua chuo hicho cha Ushoni cha ujasiri amali cha  Kibweni Mwalimu  wa chuo hicho Bibi Subira Haji Yahya alimueleza Balozi Seif kwamba lengo la kuanzishwa kwa chuo ni kuwajengea mazingira ya ajira vijana wa Shehia hiyo.
Bibi Subira alieleza kwamba mfumo huo wa mafunzo mbali ya kutengeneza kazi za ajira lakini pia utasaidia kupunguza wimbi la vitendo viovu wanavyojihusisha zaidi vijana ndani ya mitaa na kuleta kero na fadhaa kwa jamii.
Chuo cha ushoni cha ujasiri amali cha Kwa Botoro kilichoanzishwa na jumuiya ya Vijana wa Kibweni { Kibweni Yourth Organization – KYO } kimeanzishwa karibu miezi Tisa iliyopita kikiwa na wanafunzi 16 wa rika mbali mbali.
Wanafunzi wa chuo hicho hupata fursa ya kujifunza ushoni wa nguo tofauti wakianzi na zile za watoto wadogo kwa hatua ya ukataji na kufuatia ushoni utakaoambatana na kupatiwa vyeti wakati wanalizapo muda wao wa mafunzo.
Uongozi wa chuo hicho pia umeweka utaratibu wa kuwarahisishia wanafunzi wake muda wa mafunzo kulingana na harakati zao za maisha za kila siku ambapo pia hupata wasaa wa kujifunza lugha ya Kiingereza pamoja na upandaji miti katika maeneo ya vianzio vya maji vya Mwanyanya.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
9/9/2013.


Hasara ya zaidi ya Shilingi Bilioni Moja Nukta 2 imepatikana kufuatia kuungua kwa moto hoteli mbili za Kitalii za  White Sand na Sun Set Bungalows ziliopo katika Kijiji cha Kendwa Nungwi Wilaya ya Kaskazini “ A” Mkoa wa Kaskazini Unguja juzi majira ya saa 11.00 za jioni.
Hoteli ya Sun Set Bungalows inakadiriwa kupata hasara ya zaidi ya shilingi Milioni mia 400,000,000/- wakati ile ya White Sand  iliyoungua zaidi kutokana na moto huo inakadiriwa hasara ya zaidi ya shilingi Milioni mia 800,000,000/-.
Moto huo ulisababishwa na hitilafu za umeme katika moja ya majengo ya Hoteli ya Sun Set Bungalows iliyoezekwa makuti na kutoa cheche za moto zilizosambaa kwa haraka katika baadhi ya  majengo mengine kutokana na upepo mkali uliokuwa ukivuma katika eneo hilo.
Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar  Balozi Seif Ali Iddi akitokea Bungeni Mjini Dodoma alifika eneo hilo la tokeo ili kuwafariji Wamiliki, Wafanyakazi wa Hoteli hizo pamoja na Wananachi wanaozizunguuka Hoteli hizo kutokana na maafa hayo makubwa kwa uchumi wa Taifa.
Akitoa ufafanuzi wa  mkasa halizi wa tukio hilo  Mmiliki wa Hoteli ya Sun Set Bungalows Abdullsamad Ahmed Said alimueleza Balozi Seif kwamba Moto huo umevikumba vyumba Vinane vya  kulala wageni, Stoo pamoja na jiko la kupikia.
Abdullsamad alisema Wageni wapatao sabini waliokuwemo kwenye vyumba vya Hoteli hiyo waliweza kuokolewa kwa ushirikiano kati ya Wafanyakazi wa Hoteli hiyo na Wananchi walioizunguuka Hoteli hiyo jambo ambalo lilileta faraja kwa Uongozi pamoja na wafanyakazi wake.
Mmiliki huyo wa Hoteli ya Sun Set Bungalows aliwashukuru wananchi hao, Viongozi wa Serikali Wilaya na Mkoa wa Kaskazini Unguja pamoja na Maafisa wa Kamisheni ya Utalii kwa msaada wao ulichangia kupunguza machungu ya janga hilo.
Balozi Seif Ali Iddi akikagua hali ya tukio  la moto huo ambao pia uliathiri Hoteli nyengine ya jirani ya White Sand ambapo Mmoja miongoni mwa  Viongozi wa Hoteli hiyo Ramadhan Msanif  alimfahamisha Balozi Seif kwamba  wakati wakijiandaa kutoa msaada kwa wenzao jirani wa Sun Set cheche za moto huo pia zikaanza kuvamia Hoteli yao na kulazimika kukabiliana nalo.
Bwana Msanif  alisema licha ya juhudi walizochukua kukabiliana na moto huo lakini kasi kubwa ya upepo uliokuwa ukivuma wakati huo ulisababisha kuathiri  mapaa ya nyumba  10  za hoteli hiyo katika kipindi kifupi kwa vile zilikuwa na mapaa ya makuti.
Akizungumza na Viongozi, Wafanyakazi wa Hoateli hizo pamoja na Wananchi wa jirani na Hoteli hizo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif  alitoa wito kwa wananchi kuendelea kusaidia wawekezaji wakati yanapotokea majanga kwenye maeneo ya vitega uchumi.
Balozi Seif alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bado inasisitiza na kutegemea sekta ya Utalii ambayo kwa sasa inasaidia kuongeza mapato ya Taifa sambamba na kutoa ajira kwa wananachi wanaovizunguuka vitega uchumi hivyo.
Hata Hivyo Balozi Seif aliendelea kuwakumbusha wawekezaji vitega uchumi mbali mbali Nchini kujenga utamaduni wa kuiwekeza Bima Miradi yao ili wakati wanapopatwa na majanga au maafa Bima hizo ziweze kuwasaidia.
Alisema inasikitisha kuona ipo miradi ya kiwango kikubwa cha fedha inayoendelea kuwekezwa Nchini lakini wamiliki wengi wa miradi hiyo wanashinda kuikatia bima na hatiame inakufa kabisa pale inapokumbwa na majanga kama ya moto.
“ Wawekezaji na hata Wafanyabiasharawengi  bado wamekuwa wazito kuiwekea Bima miradi yao na kusahau kwa kuona ghali  mpango huo ambao kumbe huwa unawasaidia wakati wanapopatwa na majanga “. Alifafanua Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza Wananchi waliopo jirani na Hoteli hizo kwa juhudi kubwa waliyochukuwa na kusababisha  kupungua  kwa hasara kubwa iliyokuwa izikumbe hoteli hizo.
Alisema juhudi hizo zilizowaongezea nguvu za uokozi wafanyakazi wa hoteli hizo zimesaidia kuokoa mali na vifaa vya hoteli pamoja na wageni waliokuwa wakipata huduma ndani ya Hoteli hizo.
“ Nafarajika kusikia kwamba harakati za uokozi wa mali na vifaa katika Hoteli hizi mbili za White Sand na Sun Set Bungalows za Kendwa hakukuwa na ripoti za udokozi wa mali kama zilivyotokea Kwenye Hoteli ya Paradise Beach Resort iliyopo  Marumbi wakati ilipowaka moto wiki moja na nusu iliyopita.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliushauri Uongozi wa Hoteli hizo kufikiria kubadilika  katika mfumo wa ujenzi wa mapaa ya makuti ili kujilinda na  majanga yanayoweza kuepukwa licha ya kwamba mfumo huo hutoa ajira kwa wananchi wanaouza makuti yao.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliangalia eneo lililopembezoni mwa Bara bara mbele ya Skuli ya Msingi na Sekondari ya Mto Pepo ambalo liko katika hali mbaya kimazingira.
Ziara hiyo ya ghafla ya Balozi Seif ilikuja kufutia baadhi ya wananchi kufanya Biashara katika eneo hilo linalotishia afya za Binaadamu kutokana na kutuwama kwa maji machafu yanayoweza kusababisha maradhi ya kuambukiza.
Katika kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimuagiza Sheha wa Shehia ya Mto Pepo pamoja na Diwani wa Wadi ya eneo hilo kufika Ofisini kwake Vuga Jumatatu  ya Tarehe  9 Septemba  asubuhi kulijadili suala hilo.
Hali ya mazingira ya  eneo hilo mbali ya kutoa  sura mbaya kwa wapita njia na wageni lakini pia inaweza kusababisha mripuko wa maradhi  hasa kwa  wanafunzi wadogo wasiozingatia afya zao wa Skuli ya jirani na eneo hilo.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
8/9/2013.